Monday, January 14, 2008

Mserbia mwingine atua Jangwani

KLABU ya Yanga ya Dar es Salaam imemleta kocha mpya, Zivojnov Srdan kwa ajili ya timu ya vijana.

Zivojnov Srdan (35) raia wa Serbia, aliwasili nchini juzi na anatarajia kuingia mkataba wa kukinoa kikosi hicho cha vijana cha Yanga mapema wiki hii.

Mwenyekiti wa Yanga, Imani Madega alisema ujio wa kocha huyo ni faraja kubwa kwao kwani wataachana na dhana ya kugombea wachezaji na mahasimu wao, Simba.

"Atazunguka kutafuta wachezaji atakaona wanafaa kuanzia wale wenye umri kati ya miaka 12 na 14 na atakuwa na wakati mzuri kuwatengeneza," alisema Madega.

Akizungumzia hatma ya Jacky Chamangwana na wachezaji wake ambao tayari walishawachagua, mfadhili wa Yanga Yusuf Manji alisema: "Chamangwana atabaki na timu yake ile tuliiandaa kutekeleza kanuni za TFF za kutaka kuwa na timu ya vijana, yake ni ya U 20 ataendelea nayo hii ya U 14 kocha Srdan atakuwa nayo," alisema.

Manji alisema kwa hali hiyo Uwanja wa Kaunda unatakiwa kuharakishwa ujenzi wake ili timu zake za vijana ziwe zinafanya mazoezi pale hata ikibidi kukarabatiwa usiku na mchana, alisema.

MWANANCHI

No comments: