Wednesday, June 23, 2010

Wagombea waliochujwa Yanga SC watajwa

KAMATI ya uchaguzi ya klabu ya Yanga, imewaengua wagombea sita kwenye kinyang’anyiro cha kuwania uongozi wa klabu hiyo uliopangwa kufanyika Julai 18, wote ni wale waliokuwa wakiwania nafasi ya ujumbe.

Kwa mujibu wa ofisa habari wa klabu hiyo, Louis Sendeu, uamuzi huo umefanywa na kamati hiyo iliyo chini ya Jaji Mstaafu, John Mkwawa, iliyokutana juzi kutokana na wahusika kushindwa kuwasilisha vivuli vya vyeti vyao.

Walioenguliwa kutokana na dosari hiyo ni Seif Mohammed, Saburi Saburi, Edson Mandemane, Abas Bomba, Awadhi Mrido na Ahmed Mamba ambao wote walikuwa wakiwania nafasi ya ujumbe wa Kamati ya Utendaji.

Kwa nafasi ya Mwenyekiti, Sendeu alisema wagombea wote sita waliokuwa wamejitosa katika nafasi hiyo, wamepita katika hatua hiyo ya awali, wanne kwa nafasi ya Makamu Mwenyekiti huku wa nafasi ya ujumbe wakibaki 30.

Alisema baada ya mchujo huo, kuanzia leo hadi Juni 26, ni kipindi cha kuwasilisha pingamizi dhidi ya wagombea.

Kwa maamuzi hayo, wagombea wa nafasi ya Mwenyekiti ni Francis Kifukwe, Mbaraka Igangula, Llyod Nchunga, Kanali mstaafu Ali Hassan Mwanakatwe, Abeid Falcon na Edgar Chubira.

Nafasi ya Makamu Mwenyekiti, inawaniwa na Davis Mosha, Hashim Lundenga, Ayoub Nyenzi na Constatine Maligo aliyewahi kuwa Katibu Mkuu katika uongozi wa marehemu Rashid Ngozoma Matunda.

Waliobaki kwa nafasi ya Ujumbe ni Isaac Mazwila, Theonest Rutashoborwa, David Mlangwa, Majid Simba, Dk. Evance Matee, Fundi mchundo Paul Malume, Paschal Kihanga, Salum Rupia na Ramadhan Kampira, Ismail Idrissa, Omary Ndula, Yusuf Yasin, Ally Mayai Tembele, Ally Bwamkuu, Sarah Ramadhan.

Wamo pia George Manyama, Atufigwege Mwakatumbula, Mwinyi Mangara, Lameck Nyambaya, Robert Kasela, Tito Ossoro, Hamis Ambari, Shaban Mohamed, Mzee Yusuf, Dk. David Luago, Edger Fongo, Mohamed Bhinda, Tony Magale, Jackson Mresi na David Ngarafi.

Kwa mujibu wa ratiba, Juni 27 itakuwa ni Kamati kupitia pingamizi, usaili utafanyika Juni 28 na siku inayofuata, ni siku ya kutangazwa kwa wagombea. Julai 5 hadi 7 itakuwa kipindi cha kukata rufaa na kufuatiwa na kampeni.

Katika hatua nyingine Sendeu alisema uongozi umewatema rasmi wachezaji wake Amir Maftah na Jama Mba huku wakiendelea na kuzungumza na wachezaji waliomaliza mkataba wa kukipiga katika timu hiyo kwa ajili ya kusaini tena kwa msimu ujao.

No comments: