Saturday, April 21, 2007

Tumetolewa lakini bado makamuzi yataendelea Afrika

Yanga imetolewa katika michuano ya Klabu Bingwa ya Afrika baada ya kutoka sare ya 0-0 katika mchezo wa marudiano wa raundi ya 3 iliyochezwa katika Uwanja wa CCM Kirumba Jijini Mwanza. Yanga ilikuwa ikihitaji ushindi wa 4-0 ili iweze kusonga mbele katika michuano hiyo.

Yanga haikuonekana kuchangamka hasa katika kipindi cha kwanza ambapo walikuwa wanacheza kama wapinzani wao ambao hawakuwa na presha sana licha ya kucheza pungufu baada ya mchezaji wao Lachkham Chakib kupewa kadi nyekundu katika dakika ya 25 ya mchezo.

Mabadiliko yaliyofanywa katika kipindi cha pili na Kocha Micho ya kumtoa Gaudence Mwaikimba, Abdul Mtiro na Amir Maftah na nafasi zao kuchukuliwa na Mrisho Ngassa, Gula Joshua na Abuu Ramadhani angalau ilileta uhai katika mashambulizi lakini hadithi iliendelea kubaki 0-0 hadi dk 90 zinamalizika.

Katika mchezo huo, Yanga ilimchezesha Kipa Benjamin Haule huku kipa wa aliyekuwa anapewa nafasi kubwa Ivo Mapunda akiwa katika benchi la wachezaji wa akiba. Wachezaji wengine waliowakilisha Yanga katika mchezo huo ni Benjamin Haule, Shadrack Nsajigwa, Abdul Mtiro/Gula Joshua, Nadir Haroub, Wisdom Ndhlovu, Edwin Mukenya, Credo Mwaipopo, Amir Maftah/Abuu Ramadhani, Thomas Mourice, Gaudence Mwaikimba/Mrisho Ngassa na Abdi Kassim.

Yanga sasa itaingia kwenye michuano ya Kombe la Shirikisho Afrika ambapo sasa itaingia moja kwa moja katika Raundi ya 4 ya michuano hiyo na itakumbana na mshidi kati ya Al Merreikh ya Sudan na ASO Chlef ya Algeria.

Tusikate tamaa, makamuzi yataendelea. NIA TUNAYO NA SABABU TUNAYO. ALUTA CONTINUA.

3 comments:

Anonymous said...

Inauma sana jamani!
Mi naona viongozi wa chama letu hawatii bidii kuiandaa timu. Kimsingi mechi ya nyumbani huwa ni ya makamuzi na ugenini kutafuta mabao bila kujali mtafungwa ngapi! Lakini wapi, longolongo nyiiiiingi.
Anyway, tunakutana na El-Merek. Sasa hata hiyo jamani itushinde?

Anonymous said...

Hapa bwan tusidanganyane. Watanzania tumezoea longolongo tu mpira hakuna. Yaani tuliamini kabisa kuwa tutaweza kumfunga hii timu zaidi ya magoli 4 bila ya wao kuona nyavu zetu? Tutakapoanza kuwa wakweli ndio mpira wetu nao utakuwa. Micho nae ni msanii tu!! Alituahidi kuwa lazima tutashinda hi mechi hata kama tutatolewa sasa yapo wapi? Huyu sio kocha bali ni mwalimu wa nidhamu. Kazi yake hasa ni kuwafungia wachezaji. Mchezaji kucheza rafu ni sehemu ya mpira, sasa wewe unaenda kumfungia kisa amecheza rafu ya kijinga. Wachezaji wataacha kucheza jihadi kisa mwalimu wa nidhamu (Micho) atawafungia. Bora tujirudie kwenye makombe ya nyumbani kwani huku ndiko tulikozoea. El-Merreikh hatuwaezi kabisa.

Anonymous said...

Kukata Tamaa ktk maisha ni sawa na kujinyonga. Sasa wewe Anony hapo juu ulitaka Micho asemeje..? tayari tumetolewa kwa hiyo tunaenda uwanjani kukamilisha ratiba..?

Yeye akiwa kama mwalimu, ilikuwa lazima awape moyo wachezaji kuwa tunaweza kushinda ili wachezaji wajitume kutafuta ushindi. Hata hivyo alisema kazi iliyo mbele ilikuwa sawa na kuvuka mlima kilimanjaro... kwa hiyo sioni cha kumlaumu Micho.

Timu ilicheza kadiri ya uwezo wao. Kushindwa kuifunga Esperance nadhani kumetokana na ile tofauti ya soka la Tanzania na Tunisia. Wakati Tunisia ni ya 44 kwa soka duniani, Tanzania ni ya 116 kwa sasa (according to FIFA rankings). Hivyo kazi iliyo mbele yetu ni kukuza kiwango cha soka la nchi yetu, angalau ifike kwenye namba 80 duniani. hapo ndo tunaweza kushindana with confidence na hawa jamaa.

Suala la Micho kuwa kocha wa nidhamu... naamini soka ni mchezo wa nidhamu mahali popote duniani. Kaangalie movie ya GOAL (http://www.bvimovies.com/uk/goal/main.html?lang=uk) na pia (http://www.bvimovies.com/uk/goal2/index.html) uone jinsi nidhanu inavyochukuliwa na wenzetu. Hata Mastaa kama Ronaldinho na Christiano Ronaldo wanajua nidhamu na hawafanyi uzembe hata mara moja.

Micho anataka kuwajenga wachezaji wetu wa-behave kama professionals. Wawe na tofauti na wafanyakazi wa serikali yetu ambapo mtu anaingia ofisini saa 4 na saa 6 anaomba ruhusa mara kauguliwa mara kafiwa... basi kila siku visingizio. Professionals wanaweka mpira mbele, mambo mengine yote yanafuata baadaye. Tunatakiwa kumpa ushirikiano kocha wetu katika hili badala ya kumkatisha tamaa eti wachezaji wetu watashindwa kucheza sababu ya nidhamu. Atakayeshindwa bora aanze mbele... sababu tunataka mwakani na miaka ijayo tukicheza tena na Esperance tumpige na yeye goli 3.... Bila timu yenye nidhanu hatuwezi kufika huko.