Tuesday, April 27, 2010

Papic kujifunga Yanga hadi 2011
KOCHA Mserbia, Kostadin “Bill Clinton” Papic amebadilisha uamuzi wake wa kuikacha Yanga baada ya kukubali kusaini mkataba mwingine wa mwaka moja na klabu hiyo ya mtaa wa Jangwani na Twiga.

Kwa mujibu wa taarifa zilizopatikana jana zinasema kwamba kocha Papic amekubali kusaini mkataba wa mwaka moja utakaoanza mwezi ujao ikiwa ni wiki moja tangu alipotangaza kuikacha klabu hiyo kwa kushindwa kumlipa mshahara.

Papic alichukua uamuzi huo baada ya kukutana na viongozi wa klabu hiyo kujadili kwa undani kuhusu malipo yake.

Kiongozi mmoja wa Yanga, alisema Papic alikutana na mfadhili Yusuf Manji na kukubaliana kuyamaliza matatizo yake yote yaliyojitokeza kwenye mkataba wake wa kwanza.

Moja ya matatizo ni madai yake ya mshahara na malalamiko yake ya kutoheshimwa. Tangu alipokataa kuongeza mkataba wake mwaka jana mwezi Oktoba.

Mserbia huyo anategemea kusaini mkataba mpya mapema wiki ijayo utakaodumu hadi Mei 2011, kwa mujibu wa chanzo hicho cha habari.

Kwa habari zaidi endelea hapa.

Wednesday, April 21, 2010

Yanga kuishusha Prisons leo?

VILIO au vicheko vitakavyotawala leo katika majiji ya Mwanza na Mbeya baada ya filimbi ya mwisho kupulizwa wakati timu za Toto African na Prisons zitapotupa karatazao za mwisho za kubaki Ligi Kuu Vodacom Tanzania Bara kwa msimu mwingine.

Mechi nyingi za leo zinachukuliwa kama za kukamilisha ratiba ya ligi kwa timu nyingi isipokuwa kwa Toto African, Prisons na Manyema ambapo ni klabu moja tu inayoweza kujinasua kutoka kwenye janga la kushuka daraja msimu huu baada ya Moro United kuaga mapema.

Maafande wa Prisons na Toto African wote wana jumla ya Pointi 20 kila mmoja huku Manyema Rangers ikiwa juu yao kwa tofauti ya pointi mbili zaidi. Manyema wenye kibarua kizito dhidi ya Azam watakuwa wakiomba Prisons na Toto zipoteze mechi zao ili ibaki kwenye ligi.

Prisons ikishinda itafikisha pointi 23 na itakuwa mbele ya Manyema yenye pointi 22 na Toto African pointi 20,hivyo Manyema na Toto kuungana na Moro yenye pointi 15 kushuka daraja.
Prisons watakuwa kwenye uwanja wa Sokoine kuikabili Yanga. Wakati Toto watakuwa ugenini mjini Bukoba kwenye Uwanja wa Kaitaba kuwakabili wenyeji Kagera Sugar wenye pointi 23 ambao matokeo mabaya ya mchezo huo yanaweza kuwashusha daraja.

Endapo timu hizi tatu za mwisho zote zikishinda kwenye michezo yao Toto itafikisha pointi 23 kama Prisons ikishinda, lakini Manyema Rangers watanusurika kushuka daraja kwa kufikisha pointi 25.

Lakini hali hiyo inaweza kuchukua sura mpya kama Toto wataiifunga Kagera Sugar, Manyema wakatoka suluhu na Azam, huku Prisons wakiichapa Yanga mabao mawili timu zote nne za mwisho zitafikisha pointi 23.

Kwa kuwa Toto imeshafunga mabao 23, Manyema 20, Prisons 18 wakati Kagera imeziona nyavu mara 14 tu.

Hapo ndipo Kagera Sugar na Manyema Rangers zitakapoungana na Moro United kushuka daraja kwa kutumia sheria ya mabao mengi ya kushinda katika kuamua.
MSIMAMO WA LIGI MSIMU WA 2009/10

Friday, April 16, 2010

Pambano sasa kupigwa jioni

Hatimaye pambano la watani wa jadi Yanga na Simba limerudishwa nyuma na sasa litaanza saa 10.30 jioni badala ya saa 2 usiku.

Saturday, April 10, 2010

Mapato yazipeleka Yanga, Simba Aprili 18

SUALA la mapato limeendelea kutia dosari soka ya Tanzania baada ya serikali kuingilia kati na kuahirisha mechi ya watani wa jadi, Yanga na Simba lililokuwa ichezwe kesho kwenye Uwanja wa Uhuru jijini Dar es Salaam sasa utachezwa Jumapili ijayo.

Kwa habari zaidi cheki hapa

Tuesday, April 06, 2010

Tegete atarudi Ulaya?
Dili la mshambulijaji wa Yanga Jerry Tegete kucheza soka la kulipwa huko Sweden, limeota mbawa baada ya klabu yake kumtaka arejee nchini licha ya kufaulu majaribio.

Tegete ambaye aliondoka nchini Machi 18 mwaka huu, alitua katika klabu ya Dalkurd FF ya Sweden kufanyiwa majaribio ambayo alifaulu na klabu hiyo kumtaka ajiunge na nayo kwa mkopo wa miezi mitatu.

Awali wakala wa mchezaji huyo Bw. Damas Ndumbaro alitoa taarifa kwamba mchezaji huyo atarejea baada ya wiki mbili lakini wakati wiki mbili zikikaribia kumalizika, Ndumbaro aliiarifu Yanga kwamba mchezaji huyo amefaulu majaribio na klabu hiyo inaomba abaki huko Sweden ili ajiunge na Dalkurd FF kwa mkopo wa miezi mitatu.

Baada ya taarifa hiyo, klabu ya Yanga ilikataa ofa hiyo na kumtaka mchezaji huyo arejee nchini ili mazungumzo yafanyike. Yanga inadai kwamba makubaliano yalikuwa ni majaribio ya wiki mbili kisha mchezaji huyo arejee nchini kuitumikia klabu yake katika mechi mbili zilizosalia za ligi kuu ya Vodacom.

Hata hivyo tayari Ndumbaro alikaririwa na redio moja nchini akisema kwamba dili hilo la Tegete limekufa na mchezaji huyo atarejea nchini katikati ya wiki.

Mapema mwaka jana mchezaji mwingine Mrisho Ngassa aliwekewa ngumu na uongozi wa klabu hiyo baada ya wakala wa mchezaji huyo kumtafutia timu huko Norway - Lovham FC lakini Yanga ikataka taratibu zifuatwe.

Pia katikati ya miaka ya 90 mchezaji Edibiliy Lunyamila alirejeshwa nchini kutoka kwenye majaribio huko Ujerumani ili aikabili Simba katika mechi ya ligi. Baada ya mechi hiyo Lunyamila hakubahatika tena kucheza soka la kulipwa nje ya nchi.